Taarifa ya Mafanikio ya Utekelezaji
DESEMBA 2005 HADI DESEMBA 2009
TAARIFA YA MAFANIKIO YA UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU YA WIZARA KWA KIPINDI CHA MIAKA MINNE KATI YA DESEMBA 2005 HADI DESEMBA 2009
1.0 UTANGULIZI
1.1 Dira
Kuwa mlezi na msimamizi wa uhakika wa Hakimiliki ya ardhi, nyumba bora zenye hadhi na makazi endelevu kwa ajili ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
1.2 Dhima
Kuweka mazingira yanayofaa na kuleta ufanisi katika utoaji wa huduma za ardhi, nyumba na makazi kwa ajili ya maendeleo ya wateja kijamii na kiuchumi.
1.3 Misingi ya Utekelezaji wa Majukumu ya Wizara Wizara iliendelea kutekeleza shughuli zake kwa kuzingatia Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2025, Malengo ya Milenia (MDGs), Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kuondoa Umaskini (MKUKUTA) na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2005. Mambo ya Msingi yalioanishwa katika miongozo hiyo yanalenga kuboresha maisha ya wananchi; kudumisha amani, utulivu na umoja; kudumisha utawala bora; kujenga uchumi madhubuti na endelevu; kuboresha afya; mazingira na kuwa na makazi endelevu.